Rais Kikwete, akiwa anazungumza na Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Marekani John Kerry |
SERIKALI ya awamu ya nne inajivunia mafanikio iliyoyapata
tangu kuingia madarakani mwaka 2005 na kuweka msingi imara wa nchi katika
kutekeleza mkakati wa maendeleo wa mwaka
2025 unaolenga kuifanya Tanzania
kuwa nchi yenye uchumi wa kati ifikapo
mwaka 2025.
Rais Jakaya Kikwete alitoa kauli hiyo juzi jijini Washington
DC wakati akitoa mhadhara katika Kituo cha Kimataifa cha Woodrow Wilson.
"Naamini mrithi wangu atayaendeleza na kujifunza
kutokana na mafanikio haya na kuendeleza kutoka pale tutakapoachia,"
alisema.
Rais Kikwete, alisema anatarajia Tanzania itakuwa na sera na sheria ya
kusimamia gesi na mapato yake kwa vile inatarajiwa kuanza kupatikana ifikapo
mwaka 2020.
Katika mhadhara huo uliohudhuriwa na watu mbalimbali
wakiwemo mabalozi, wasomi na viongozi wa taasisi hiyo, Rais Kikwete alielezea mafanikio na changamoto
katika uongozi wake wa miaka 10 katika elimu, siasa, uchumi na maendeleo ya
jamii.
"Najivunia kuweza kuendelea kuliweka Taifa katika hali
ya umoja pamoja na changamoto zote, tumepambana na vitisho pale vilipojitokeza
na pia tumetoa mchango mkubwa katika harakati za kisiasa zilizopelekea vyama
viwili kutiliana saini maridhiano na kupata muafaka mwaka 2010," alisema.
Rais Kikwete alisema makubaliano hayo yalipelekea Zanzibar
kufanya uchaguzi kwa amani na kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa baina ya
vyama vya CCM na CUF.
"Natumaini tutafanya uchaguzi huru, haki na aman,i ili niweze kumkabidhi
urais mrithi wangu katika hali ya utulivu"
alisema Rais.
No comments:
Post a Comment