KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Tuesday 28 April 2015

SITTA AHOFU KUTOKEA VURUGU KAMA KATIBA PENDEKEZWA HAITAPITISHWA


Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta

WAZIRI wa Uchukuzi, Samuel Sitta, ameonyesha wasiwasi wake kuwa iwapo Katiba inayopendekezwa haitapitishwa na kuchangia Uchaguzi Mkuu kufanyika kwa kufuata Katiba ya zamani, kuna uwezekano wa kutokea vurugu katika uchaguzi huo unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.
Akifungua mkutano wa Baraza la Wafanyakazi wa wizara hiyo uliofanyika jana jijini Dar es Salaam, Sitta alisema wapo baadhi ya Watanzania wanaoikataa Katiba hiyo bila kueleza mbadala wake uliko.
 “Unapokikataa kitu ni lazima ueleze mbadala wa kitu unacho kikataa ni nini, na unaposema Katiba hii ni batili, tueleze iko wapi ambayo si batili. Katiba hii isipopitishwa na tukaenda kwenye uchaguzi kwa Katiba ya zamani, bila shaka tunaandaa vurugu nchini ambazo hazina sababu,” alisema.
Sitta alisema kuwa kundi linalopinga Katiba inayopendekezwa ndilo lililokuwa la kwanza kupinga Katiba inayotumika sasa.
“Watu wanaoikataa Katiba inayopendekezwa ndio walewale waliokuwa wanaikataa kwa nguvu zote Katiba inayotumika hivi sasa…hao hao ndio watakaogeuka baadaye kupinga matokeo ya uchaguzi kwa madai Katiba iliyotumika haikuwa na sifa,” alisema Sitta.
Aliwataka wajumbe wa baraza hilo kuisoma vema Katiba inayopendekezwa ili waweze kuipigia kura kutokana na kuwa na masuala ya msingi na yenye masilahi kwa taifa.
Mkutano huo ulikuwa mahususi kwa ajili ya kuwachagua katibu na msaidizi wa baraza hilo pamoja na kujadili maandalizi ya bajeti ya wizara hiyo inayotarajiwa kujadiliwa kwenye Bunge la Bajeti linalotarajiwa kufanyika mwezi ujao.
Awali akimkaribisha Sitta, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Shaaban Mwinjaka, alisema wizara hiyo imekuwa na changamoto kubwa ya bajeti finyu ambayo inayumbisha baadhi ya kazi za wizara hiyo na kushindwa kutekelezwa.
Akitoa mfano wa kwenye sekta ya anga, Mwinjaka alisema walipeleka maombi ya fedha kwa ajili ya kununua rada za kuongoza ndege mbili, ambayo Tume ya Mipango iliyapitisha, lakini hadi leo hawajaingiziwa fedha.
“Tanzania pamoja na ukubwa wake huu ina rada moja tu, na hii si nzuri kwa masuala ya usalama kwenye sekta hii, hasa ukilinganisha na jirani zetu kama Kenya, wana rada sita, Burundi na Rwanda zaidi ya rada nne lakini sisi rada moja, hii si sawa,” alifafanua.

No comments:

Post a Comment