KAMA UNA TUKIO LOLOTE LA KIJAMII, SIASA, UCHUMI TUWASILIANE KWA E-mail: shehesemtawa@gmail.com SIMU: 0719 352 268

Tuesday 28 July 2015

JAJI MALABA: FOMU ZA URAIS AGOSTI MOSI

Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula (kushoto), akifurahia jambo na Katibu Mkuu wa NRA, Hassan Almasi, (katikati) na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Salum Mwalimu, baada ya kusaini maadili ya uchaguzi yaliyoandaliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwa ushirikiano na wadau wake jijini Dar es Salaam jana.
TUME  ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imesema fomu za kuwania nafasi ya urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zitaanza kutolewa Agosti Mosi mwaka huu.
Kauli hiyo ilitolewa jijini Dar es Salaam jana na Mwenyekiti wa NEC, Jaji mstaafu Damian Lubuva alipozungumza na waandishi wa habari  baada ya mkutano wa utiaji saini na vyama  vya siasa katika Kitabu cha Maadili ya Uchaguzi Mkuu.
Jaji Lubuva alitoa kauli hiyo baada ya kuulizwa swali NEC itaanza lini kutoa fomu za kuwania urais katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 25 mwaka huu.
Alisema licha ya NEC kuanza kugawa fomu hizo za rais katika kipindi hicho, pia fomu za wabunge zitatolewa Agosti 8 mwaka huu.
Akizungumzia utiaji saini katika kitabu cha maadili ya uchaguzi wa rais, wabunge na madiwani, alisema tume imekubaliana na vyama vyote 21 vilivyohudhuria mkutano huo wa utiaji saini katika kitabu hicho isipokuwa Chama cha Wananchi (CUF).
“Tumekubaliana baada ya kupitia maeneo mbalimbali ambayo yalikuwa yakiihusu tume na kwa upande mwingine vyama vya siasa, baadaye wote wakaridhia kuyatia saini,”alisema Jaji Lubuva.
Alisema CUF kimeshindwa kutokea katika utiaji saini huo kutokana na kukakabiliwa na majukumu mengine na kusema kuwa chama hicho bado kina muda na wakati wowote kinaweza kwenda kufanya hivyo.
Jaji Lubuva alisema wahusika wakuu wa maadili hayo ni vyama vya siasa, wagombea, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na NEC, ambapo kila chama na mgombea atawajibika kusaini maadili hayo.
“Chama ambacho hakitasaini maadili haya kitazuiliwa kushiriki katika kampeni za uchaguzi,”alisema Jaji Lubuva.
Alisema kuwa kila mgombea atajaza na kusaini fomu na. 10 kuthibitisha kuwa ataheshimu na kutekeleza maadili hayo na kwamba fomu hiyo itatolewa na NEC na kurudishwa pamoja na fomu ya uteuzi.
Akizungumzia kipengele cha mawasiliano ambacho kinasema hakuna mtu atakayeruhusiwa kutumia simu ya kiganjani ndani ya kituo cha kupigia, kuhesabia na kujumlishia kura isipokuwa msimamizi wa kituo, wasaidizi wake na mlinzi wa kituo cha kupigia kura.
“Watu hao watatumia simu zao pale itakapobidi kwa shughuli za uchaguzi tu na simu hizo wakati wote ziwe zimeondolewa mlio na ziwe kwenye mtetemo,”alisema Jaji Lubuva.
Hata hivyo, baada ya mvutano kuhusu kipengele hicho, NEC na vyama walikubaliana mawakala waingie na simu, lakini wakati wote ziwe katika mtetemo huku mhusika atakapohitaji kufanya mawasiliano atoke nje.
Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Salum Mwalimu alisema kipengele hicho kimerekebishwa na kwamba kila wakala ataingia na simu yake isipokuwa hawataruhusiwa kuongea ndani ya kituo cha kupigia kura.
Makubaliano ya kusaini kitabu hicho cha maadili wiki iliyopita yalivunjika baada ya vyama hivyo kubaini kuwa kurasa 10 kati ya 24 zilinyofolewa huku NEC ikishindwa kuwafahamisha nini kilisababisha hali hiyo.

No comments:

Post a Comment